Wananchi wa Saku wahimizwa kuchukua vitambulisho vyao vya kitaifa.
Na Abdiaziz Yusuf
Kiongozi wa vijana wa eneo bunge la Saku, Abdilaziz Boru, amewarai wakazi waliotuma maombi ya vitambulisho vya kitaifa kujitokeza kuvichukua ili kupunguza mrundikano wa vitambulisho ambavyo havijachukuliwa katika afisi za usajili.
Akizungumza na Shajara ya Radio Jangwani, Boru amesema baadhi ya vitambulisho hivyo hupelekwa katika afisi za machifu baada ya kutolewa, lakini bado wengi hawajajitokeza kuvichukua.
Aidha, amewahimiza wananchi watakaopokea vitambulisho vyao kujiandikisha kama wapiga kura ili waweze kushiriki katika uchaguzi mkuu wa mwaka ujao na kutimiza haki yao ya kidemokrasia ya kuwachagua viongozi.
Wakati huo huo, Boru amemshukuru Rais William Ruto kwa kuondoa utaratibu wa kuwafanyia vijana wa eneo la Kaskazini Mashariki usaili maalum kabla ya kupatiwa vitambulisho vya kitaifa, akisema hatua hiyo imerahisisha upatikanaji wa stakabadhi hizo muhimu.



Post Comment