Highlights

Walengwa wa HSNP kupokea malipo ya miezi miwili mwishoni mwa wiki – NDMA Marsabit

Na Samuel Kosgei

Usimamizi wa Mamlaka ya Kitaifa ya Kukabiliana na Ukame (NDMA) tawi la Marsabit umesema kuwa walengwa wa Mpango wa Hunger Safety Net Programme (HSNP) watapokea malipo ya miezi miwili mwishoni mwa wiki hii.

Mkurugenzi wa NDMA Marsabit, Golicha Guyo, amesema tayari ofisi ya HSNP imekamilisha maandalizi ya orodha ya malipo, huku walengwa wakitarajiwa kupokea fedha hizo siku ya Ijumaa au Jumamosi, kutegemea kasi ya mchakato wa benki.

Hata hivyo, Guyo amesema kuwa bado kuna malimbikizo ya malipo ya miezi sita ambayo hayajatolewa. Amesema NDMA inaendelea kushirikiana na wadau husika ili kuhakikisha fedha hizo zinatolewa haraka iwezekanavyo.

Kwa mujibu wake, Bunge tayari liliidhinisha kutolewa kwa fedha hizo, lakini Wizara ya Fedha bado haijakamilisha mchakato wa kuziwasilisha kwa utekelezaji wa malipo.

Mpango wa Hunger Safety Net Programme (HSNP) ni mpango wa Serikali unaotoa ruzuku ya fedha taslimu bila masharti kwa familia zilizo katika mazingira magumu. Mpango huo unatekelezwa na Mamlaka ya Kitaifa ya Kukabiliana na Ukame (NDMA) katika kaunti nane za ukame na umaskini ambazo ni Turkana, Wajir, Mandera, Marsabit, Garissa, Tana River, Isiolo na Samburu.

Post Comment