County Updates, Diocese of Marsabit, Local Bulletins

Visa 10 vya ugonjwa wa macho mekundu (Red Eyes) vyaripotiwa katika kaunti ya Marsabit

Waziri wa afya Grace Galmo wakati wa kikao na waandishi wa habari.
Picha: Radio Jangwani

Na Samwel Kosgei,

Wizara ya afya kaunti ya Marsabit imetangaza uwepo wa visa 10 vya ugonjwa wa macho mekundu (red eyes) ambao mwezi jana ulitangazwa kuwepo kaunti ya Mombasa.

Wizara hiyo ikiongozwa na waziri wa afya Grace Galmo imesema kuwa dalili ya ugonjwa huo ni ikiwemo kuhisi uchungu machoni, kufura macho, kujikunakuna, uwepo wa usaha na macho kuogopa mwangaza.

Akizungumza na waandishi wa habari katika hospitali kuu ya Marsabit, Galmo amewataka wananchi kuzidi kuzingatia usafi wa mikono haswa kwa kutumia maji na sabuni na pia kuweka-usafi wa hali ya juu ili kuepuka ugonjwa huo.

Wakati huo waziri Galmo ametangaza ongezeko la ugonjwa wa Malaria haswa katika maeneobunge ya Saku na Moyale. Kaunti ndogo za Laisamis na North Horr pia zimeripoti visa vya ugonjwa wa malaria kuongezeka.

Eneo la Songa na Jaldesa ndiyo yametajwa kuathirika Zaidi.

Ameitaka umma kuzidi kutumia neti ya mbu, kunyunyiza dawa ya mbu na hata kusaka matibabu mtu anapougua.

Kwenye suala la ugonjwa wa homa ya Rift Valley wizara hiyo sawa na ile ya mifugo imesema kuwa bado visa vya homa hiyo ni vinne na vyote vilipatikana katika eneo la Shurr.

Hata hivyo waziri Galmo na mkurugenzi wa huduma za chanjo ya mifugo Boku Bodha wamesema kuwa hamna wasiwasi kwani visa hivyo vimedhibitiwa.

Aidha wizara ya mifugo imetaka wananchi kuepuka kula nyama ambayo haijakagualiwa na daktari wa mifugo, kutoshika mzoga wa mifugo aliyekufa, kutoshika ndama wanaozaliwa kama siku zao hazijafika na kulala ndani ya neti ya mbu kwani binadamu wanaambukizwa homa hiyo na mbu.

Subscribe to eNewsletter