County Updates

Wakazi wa Marsabit Wapongeza Uteuzi wa Jumanne wa Kabale Tache Arero NLC

Baadhi ya wakazi wa Saku wakihutubia wanahabari Jumatano, Juni 14 2023, wamepongeza uteuzi wa Kabale Tache Arero kuhudumu NLC

Na Jacob Nateleng

Baadhi ya wakazi wa kaunti ya Marsabit wamepongeza uteuzi wa Jumanne wa Kabale Tache Arero kuwa Afisa Mkuu Mtendaji wa Tume ya Kitaifa ya Ardhi-NLC, nafasi ambayo ameshikilia kama kaimu kwa miaka mitano iliyopita.

Wakiongozwa na kiongozi wa vijana katika eneo la Saku Abdi Boru wakazi hao walimpongeza hasa rais William Ruto kwa kuwateua viongozi wa jamii ya wafugaji kushikilia nyadhifa muhimu katika serekali kuu.

Abdi alielezea matumaini kwamba hatua ya rais itasaidia pakubwa katika kusukuma ajenda za maendeleo katika kaunti hii akiwataka pia viongozi hao kuwa kielelezo chema kwa wananchi kuafikia amani na maendeleo hapa jimboni.

Mwenyekiti wa NLC Gershom Otachi katika taarifa alithibitisha kuteuliwa kwa Kabale kufuatia mchakato mkali wa uajiri ambao ulikamilika mnamo Juni 12.

Nafasi hiyo, iliyoachwa wazi kufuatia kusimamishwa kazi na hatimaye kuondoka kwa Tom Chavangi mwaka wa 2018, ilivutia watu 172 waliotuma maombi.

Aidha wakazi hao walitoa wito kwa viongozi wa kaunti ya Marsabit kuweka kando tofauti zao za kisiasa na kikabila na baadala yake kuhudumia wananchi wote wa kaunti ya Marsabit bila mapendeleo.

Subscribe to eNewsletter