County Updates, Local Bulletins

Wafanyibiashara mjini Marsait, walalamikia hatua ya maafisa wa idara ya kuzoa taka kujikokota kuondoa taka mjini.

Maafisa wa idara ya kuzoa taka wakizoa taka mjini Marsabit.
Picha;Mark Dida

By Mark Dida,

Wafanyabiashara mjini Marsait, wamelalamikia kile wanachosema ni hatua ya maafisa wa idara ya kuzoa taka katika kaunti ya Marsabit, kujikokota kuondoa taka mjini humu.

Wamesema kuwa taka hizo ambazo zimerundikana katikati ya mji, zinatoa uvundo kiasi cha kuyumbisha biashara zao.

Wanataka taka hizo kuondolewa haraka iwezekanavyo, wakisema kuwa uwepo wa taka mjini kwenye eneo la soko na uvundo mkali unahatarisha afya ya binadamu na kuwa tisho kwa mazingira.

Vile vile wametaja kuwa uwepo wa taka mara nyingi umesababisha hata ajali kutokana na msogamano mkubwa mjini, na kwamba juhudi zao za kuomba usaidizi kwa idara ya kuzoa taka hazijazaa matunda.

Maafisa wa idara ya kuzoa taka wakizoa taka mjini Marsabit.
Picha;Mark Dida

Wamesema kuwa Marsabit ni mji mkubwa na kusisitiza umuhimu wa taka kuondolewa mjini humu kila siku, na sio baada ya siku kadhaa jinsi inavyofanyika sasa.

Kwa upande wake meneja wa manisipaa ya Marsabit Boru Golicha amesema tatizo hilo limetokea baada ya baadhi ya akina mama walioajiriwa kufanya kazi ya usafi mjini kususia kazi kutokana na kucheleweshwa kwa malimbikizi ya mishahara yao, hivyo kutatiza shughuli nzima ya kuondoa taka hizo.

Boru ameomba wakaazi wa mji wa Marsabit na viunga vyake kushirikiana na serikali ya kaunti kuhakikisha mji huu ni msafi, ili kuepusha magonjwa yatokanayo na uchafu na kuondoa picha mbaya kwa wageni wanaozuru Marsabit.

Subscribe to eNewsletter