Wanasiasa Marsabit watakiwa kuepuka kuingilia masuala ya elimu
NA JB Nateleng.
Wanasiasa katika kaunti ya Marsabit wametakiwa kujiepusha kuingilia masuala ya elimu ili kuwapa walimu nafasi ya kutekeleza majukumu yao ipasavyo.
Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa Chama cha Wazazi na Walimu (PTA) jimboni Marsabit Ali Noor, kumekuwepo na visa ambapo walimu wamehamishwa kutoka shule moja hadi nyingine kutokana na kutoelewana na baadhi ya wanasiasa.
Akizungumza na Shajara, Noor amesema hali hiyo inatatiza mfumo wa elimu na kuathiri maslahi ya wanafunzi.
Na baada ya rais William Ruto kuagiza wanafunzi wote wa gredi ya 10 kuripoti shuleni hata bila karo, sare wala vifaa vya kimsingi, Noor amesema kunao baadhi ya walimu wakuu jimboni Marsabit ambao hawajatii agizo la kuwapokea na kuwaruhusu wanafunzi hao kuendelea na masomo.
Kadhalika Noor ametaja athari za ukame kama changamoto zinazochangia kudorora kwa mahudhurio ya wanafunzi shuleni.
Ametoa wito kwa serikali kuu, ile ya kaunti pamoja na mashirika yasiyo ya kiserikali kusaidi katika kukabiliana na hali hiyo ili kuhakikisha kuwa wanafunzi wanapata fursa ya kupata elimu.



Post Comment