Highlights

Wakazi wa Marsabit watoa maoni tofauti kuhusu fidia ya waathiriwa wa maandamano

Na Abdiaziz Yusuf

Baadhi ya wakazi wa Marsabit wamepinga hatua ya serikali ya kutenga shilingi bilioni mbili kufidia waathiriwa wa ukatili wa polisi na vurugu zilizoshuhudiwa wakati wa maandamano tangu mwaka 2017.

Wakizungumza na Shajara, wakazi hao wamesema kuwa fedha hizo haziwezi kurudisha maisha ya walioaga dunia. Wamedai kuwa badala ya kulipa fidia pekee, serikali inapaswa kuhakikisha maafisa wote waliohusika wanachukuliwa hatua za kisheria.

Hata hivyo, baadhi ya wakazi wameunga mkono mpango huo wakisema kuwa fedha hizo zinaweza kusaidia familia zilizoathirika, hasa katika kugharamia ada za shule na mahitaji mengine muhimu ya watoto walioachwa nyuma.

Aidha, wakazi hao wameitaka serikali kuheshimu na kulinda maisha ya wananchi wakati wa maandamano, wakisema matumizi ya nguvu kupita kiasi yanaweza kusababisha maafa na kupoteza maisha.

Post Comment