Wakazi wa Huri Hills walalamikia uuzaji wa chakula cha msaada na dhuluma za chifu
NA Nyabande Orwa
Wakazi wa eneo la Huri Hills katika kaunti ndogo ya Maikona, kaunti ya Marsabit, wamelalamikia madai ya kuuzwa kwa chakula cha msaada pamoja na dhuluma kutoka kwa afisi ya chifu wa eneo hilo.
Wakizungumza na kituo hiki mapema leo Alhamisi baada ya kuwasilisha malalamishi yao kwa Kamishna wa Kaunti, James Kamau, wakazi hao wamesema kuwa chakula cha msaada kilichotolewa mwezi Machi kilichelewa kuwafikia. Wanasema walilazimika kulalamika kwa kamishna huyo kabla ya kupata msaada mwingine.
Kwa mujibu wa mwanaharakati Ali Gorai, chifu huyo amekiuka Ibara ya Sita ya Katiba inayozungumzia uadilifu na uwajibikaji wa maafisa wa umma.
Wakazi hao sasa wametoa wito kwa Waziri wa Usalama wa Kitaifa, Kipchumba Murkomen, pamoja na maafisa wa upelelezi kuanzisha uchunguzi kuhusu tuhuma za matumizi mabaya ya ofisi na wizi wa chakula cha msaada.
Kamishna wa kaunti ya Marsabit James Kamau amedhibitisha kupata malalamishi ya wakazi hao na kuahidi kuanzisha uchunguz dhidi yanayomkabili chifu huyo ambaye jina lake tumelibana.



Post Comment