Highlights

Wahamiaji 15 raia wa Eritrea wakamatwa NorthHorr kwa kuwa nchini kinyume na sheria

NA Caroline Waforo

Wahamiaji 15 raia wa Eritrea wamekamatwa katika lokesheni ya Saru eneo bunge la North Horr kaunti ya Marsabit kwa kuwa nchini Kenya kinyume na sheria.

Akithibitisha hilo Afisa mkuu wa upelelezi katika kaunti ya Marsabit Kennedy Nyagah, amesema kuwa raia hao 15 walikamatwa tarehe 21 mwezi huu wa Januari wakisafiri kutumia gari aina ya Land Cruiser bila stakabadhi hitajika za kuwaruhusu kuwa humu nchini Kenya.

Raia hao walifikishwa katika mahakama ya Marsabit Alhamisi wiki jana ambapo kumi walio na umri wa miaka 18 na zaidi, walipigwa faini ya shilingi elfu 70 au kifungo cha miezi mitano jela huku wengine watano wa chini ya umri wa miaka 18 wakiachiliwa huru.

Vilevile dereva anayetuhumiwa kuwasafirisha wahamiaji hao, ambaye ni raia wa Kenya, alikamatwa na kuwasilishwa katika mahakama hiyo ya Marsabit ambapo alikana mashtaka dhidi yake na kuachiliwa kwa bondi ya shilingi milioni 1 au dhamana ya pesa taslimu 500,000.

Mshukiwa huyo anatarajiwa kurejea mahakamani hapo kesho Jumatano.

Post Comment