Ukavu kuendelea kushuhudiwa Marsabit katika kipindi cha siku saba- Idara ya hali ya anga yadokeza
Na Caroline Waforo
Idara ya Hali ya Hewa Kaunti ya Marsabit imetoa utabiri wa hali ya hewa kwenye ripoti yake ya kila wiki inaonyesha kuwa sehemu kubwa ya kaunti inatarajiwa kuwa kavu huku mvua zikitarajiwa kunyesha katika maeneo machache.
Kulingana na utabiri huo wa kuanzia tarehe 9 hadi 15 mwezi huu wa Juni , maeneo yatakayoshuhudia ukavu ni pamoja Marsabit mjini, Karare, North Horr, Dukana, Maikona, Turbi, Kargi, Laisamis, Loglogo, Korr, Ngurunit, Loiyangalani pamoja na maeneo mengi ya kaunti ndogo ya Moyale.
Mvua chache zitashuhudiwa katika baadhi ya maeneo machache yaliyo karibu na Mlima Marsabit, Sagante Jaldesa, Maikona, Sololo pamoja na maeneo machache yanayopakana na Ethiopia
Ukungu nyakati za asubuhi na jioni unatarajiwa kushuhudiwa katika maeneo yaliyo karibu na mlima Marsabit
Katika ukanda wa Loiyangalani na Ziwa Turkana, hali ya joto kali na upepo mkali inatarajiwa kutawala. Upepo huo unaweza kusababisha mawimbi makubwa ziwani, vumbi na kupungua kwa uwezo wa kuona.



Post Comment