Sheria ya watoto yaongeza ulinzi wa haki za watoto Marsabit.
Na Nyabande Orwa.
Sheria ya watoto ya mwaka 2022 imechangia kuimarisha ulinzi wa haki za watoto nchini. Hayo ni kwa mujibu wa hakimu mkuu mkazi wa mahakama ya Marsabit, Christine Wekesa.
Wekesa amesema kuwa kupitia sheria hiyo, mahakama imepata uwezo zaidi wa kushughulikia masuala yanayowahusu watoto. Akizungumza wakati wa uzinduzi wa maadhimisho ya siku ya mtoto wa Afrika uliofanyika Jumanne katika kaunti ya Marsabit, alisema kuwa idara ya mahakama pia imeanzisha njia mbadala za kutatua migogoro inayowahusu watoto ili kuhakikisha haki inapatikana kwa haraka.
Wakati huo huo, amesema watoto katika kaunti ya Marsabit bado wanakabiliwa na changamoto mbalimbali kutokana na athari za mabadiliko ya tabianchi ambazo zimeendelea kuathiri eneo hili.
Hata hivyo, ametoa wito kwa wadau wote kushirikiana ili kuhakikisha watoto wanalindwa na kupata haki zao kikamilifu.



Post Comment