Ongezeko la wizi wa maduka waibua wasiwasi Marsabit
Na Nyabande Orwa
Kamanda wa polisi kaunti ya Marsabit, Leonard Kimaiyo, amesema maafisa wa usalama wameimarisha doria ndani na pembezoni mwa mji wa Marsabit ili kukabiliana na ongezeko la visa vya uvunjaji wa maduka na wizi.
Akizungumza na kituo hiki, Kimaiyo amewataka wananchi wanaoathiriwa na matukio hayo kutoa taarifa kwa polisi mara moja ili hatua za kisheria ziweze kuchukuliwa dhidi ya wahusika.
Kauli yake inajiri siku chache baada ya duka lingine kuvunjwa mwishoni mwa wiki iliyopita katika eneo la Karantina, eneo bunge la Saku, ambapo wahuni walitoroka na mali inayokadiriwa kuwa na thamani ya shilingi elfu sabini.
Takriban wiki moja iliyopita, mfanyabiashara mmoja katika eneo la Wabera, viungani mwa mji wa Marsabit, alipoteza bidhaa za duka lake zenye thamani ya zaidi ya shilingi elfu hamsini baada ya duka hilo kuvamiwa na kuporwa usiku.



Post Comment