Ngamia walioibwa Wajir Magharibi warejeshwa baada ya kupatikana Laisamis.
NA Nyabande Orwa
Maafisa wa usalama katika eneo bunge la Laisamis wamefanikiwa kurejesha ngamia sita wanaodaiwa kuibiwa kutoka Wajir Magharibi wiki moja iliyopita.
Akithibitisha tukio hilo, Naibu Kamishna wa kaunti ndogo ya Laisamis, Kepha Mwaribe, amesema kuwa maafisa wa usalama kwa ushirikiano na wazee wa eneo hilo walifanikiwa kuwapata ngamia hao na kuwapeleka katika kituo cha polisi cha Laisamis.
Mwaribe amekanusha madai kuwa wezi wa mifugo walijaribu kushambulia kituo hicho cha polisi Ijumaa iliyopita, akisema kuwa mchakato wa kuwakabidhi ngamia hao kwa wamiliki wao ulifanyika kwa amani.
Wakati huo huo, ametoa wito kwa machifu kuhakikisha watoto wote wanaofaa kwenda shule wanarejea masomoni shule zitakapofunguliwa, ili kusaidia kukabiliana na visa vya wizi wa mifugo katika eneo hilo.



Post Comment