Highlights

Mbunge wa North Horr Wario Adhe aitaka vitengo vipya vya utawala Illeret kuanzishwa kwa haraka.

Na Samuel Kosgei

MBUNGE wa North Horr, Wario Guyo Adhe, ameitaka serikali kuu kuharakisha uanzishaji wa vitengo vipya vya utawala katika Kaunti Ndogo ya Illeret, akisema upungufu wa vitengo hivyo unatatiza utoaji wa huduma, uratibu wa usalama na mwitikio wa dharura.

Akizungumza bungeni, Adhe ameomba taarifa kuhusu kile alichokitaja kuwa uwepo usioridhisha wa Vitengo vya Utawala vya Serikali ya Kitaifa (NGAO) katika kaunti ndogo hiyo yenye eneo kubwa linalopakana na Ethiopia.

Mbunge huyo amesema Illeret ina ukubwa wa zaidi ya kilomita za mraba 4,000 kandokando ya mpaka wa Kenya na Ethiopia, lakini kwa sasa inahudumiwa na chifu mmoja na naibu chifu mmoja pekee. Alisema idadi hiyo ndogo ya maafisa wa utawala imeathiri shughuli za serikali na kudhoofisha utoaji wa huduma kwa wakazi.

Adhe alisema kuwa kupitia mikutano ya ushirikishwaji wa umma, wakazi walipendekeza kuanzishwa kwa Tarafa ya Telesgaye, lokesheni ya Elbokoch na Ilollo, pamoja na lekesheni ndogo ya Aibete na Lamadang. Hata hivyo, alisema vitengo hivyo bado havijachapishwa rasmi kwenye Gazeti la Serikali wala kuanza kufanya kazi.

Mbunge huyo aliitaka serikali kuharakisha uanzishaji na uendeshaji wa vitengo hivyo vya utawala, akisema hatua hiyo itaongeza uwepo wa serikali, kuimarisha usalama, kuboresha upatikanaji wa huduma za umma na kuimarisha utawala katika eneo hilo la mbali.

Aidha, Adhe alisisitiza kuwa ataendelea kutetea maendeleo yenye usawa katika eneo bunge la North Horr, akisema hakuna jamii inayopaswa kuachwa nyuma katika kupata huduma za serikali.

Post Comment