Idara ya elimu jimbo katoliki la Marsabit yakemea uharibifu wa uzio wa shule ya kukub Fam Turbi
Na JB Nateleng
Idara ya elimu ya Jimbo katoliki la Marsabit imelaani vikali tukio la kuharibiwa kwa uzio wa shule ya msingi ya Kukub Fami iliyoko Turbi, katika eneo bunge la North Horr, kaunti ya Marsabit, na watu wasiojulikana.
Akizungumza na shajara ofisini mwake, mkurugenzi wa elimu katika jimbo katoliki la Marsabit, Padri Abraham Ali, amesema waliohusika na uharibifu huo wanapaswa kukamatwa na kuwajibishwa kisheria.
Padri Abraham amesema shule ya Kukub Fam ilianzishwa na Kanisa Katoliki mwaka 2020 kwa lengo la kuwapatia watoto wa eneo la Turbi fursa ya elimu kabla ya kukabidhiwa serikali kwa ajili ya kuendelezwa akieleza kuwa uharibifu wa uzio wa shule hiyo ni kitendo kisichokubalika na kinachohujumu maendeleo ya elimu.
Aidha, Padri Abraham amesisitiza kuwa elimu ni haki ya kila mtoto na haipaswi kuingiliwa na masuala ya kisiasa akiwataka viongozi wa kisiasa kushirikiana katika kuimarisha sekta ya elimu bila ubaguzi wa eneo au dini.
Wakati huo huo, tukio hilo limeripotiwa katika kituo cha polisi cha Turbi, ambapo uchunguzi umeanza.



Post Comment