Local Bulletins

SERIKALI YAONGEZA MARUFUKU YA SIKU 30 KWENYE MIGODI 13 YA DHAHABU ILIYO ENEO LA DABEL MOYALE.

 

NA Samuel Kosgei

Serikali imetangaza upya uwepo wa marufuku ya siku 30 kwenye migodi 13 ya dhahabu iliyo eneo la Hillo, lokesheni ya Dabel eneobunge la Moyale kaunti hii ya Marsabit ikitaja maeneo hayo kuwa hatari na inayotishia.

Kamishna wa kaunti ya Marsabit James Kamau amekariri notisi ya kaimu waziri wa masuala ya ndani Musalia Mudavadi iliyoongeza marufuku ya wachimba migodi kutofika eneo hilo ambalo limetajwa kama tishio kwa usalama wa wananchi.

Kamau akizungumza nasi amesema kuwa lazima mikakati mwafaka iwekwe na serikali mwanzo kabla ya eneo hilo kufunguliwa tena. Ametaja umuhimu wa mkakati wa usalama, afya, mazingira na hata barabara kushughulikiwa mwanzo.

Amesema kuwa wiki jana idara ya usalama Marsabit ilifanya mkutano na wizara ya madini jijini Nairobi iliyojumuisha washikadau mbalimbali ikiwemo: viongozi changuliwa wa Marsabit, wazee kati wengine.

Aidha ameonya wachimba migodi dhidi ya kufika eneo hilo lililoharamishwa kwani watapatana na mikono ya serikali. Wiki jana kwenye tukio la vifo vya watu wawili – watu 34 ikiwemo wa taifa la Ethiopia walikamatwa.

Kwenye tukio la mashambulizi eneo la Sessi, Moyale wiki jana Kamau amesema uchunguzi bado unaendelea.

Idara ya polisi kwenye gazeti la serikali pia kupitia Kaimu Inspekta Jenerali wa Polisi Gilbert Masengeli alitoa notisi ya kuzuia matumizi ya silaha katika migodi ya Hillo.

Gavana wa Marsabit Mohamud Ali, Alhamisi wiki jana alilalamika kwamba licha ya kufungwa kwa migodi hiyo, uvamizi wa wachimba migodi haramu umesalia kukithiri na kusababisha makabiliano na polisi na hata maisha kupotea.

 

Subscribe to eNewsletter