Local Bulletins

IDARA YA ELIMU MARSABIT YAKANA KUWEPO KWA UPUNGUFU WA MADARASA SHULE YA CHEKECHEA YA ELEBOR WAKIITAJA KAMA SIASA

Na Caroline Waforo

Baada ya malalamishi ya wakaazi wa eneo la Elebor iliyoangaziwa na Radio Jangwani kuhusu uhaba wa madarasa katika shule ya chekechea ya Elebor iliyoko kaunti ndogo ya Sololo, idara ya elimu humu jimboni Marsabit imelaani malalamishi hayo ikiyataja kama yaliyochochewa kisiasa.

Akizungumza na shajara ya Radio Jangwani kwa njia ya kipekee Waziri wa Elimu kaunti ya Marsabit Ambaro Abdulah Ali alihoji kwanini wakaazi hao walisubiri kipindi kirefu kuibua malalamishi yao.

“Kama Idara Husika Tunalaani kitendo cha hivi maajuzi ambacho wanafunzi walipelekwa nje na kupigwa picha ili kuonekana hawana darasa. Hiyo ni siasa na tusichanganye masomo na siasa tafadhali” Alisema waziri Ambaro

Kadhalika aliwataka wakaazi hao kuibua malalamishi yao na mwakilishi wadi husika.

Hivi maajuzi wakaazi wa Elebor walilalamiakia uhaba wa madarasa wakidokeza kuwa wana darasa moja ambalo linatumiwa na wanafunzi 164 idadi ambayo imezidi uwezo wa darasa hilo.

Haya yanajiri huku pia waziri Ambaro akidokeza kuwa wapo walimu wa kutosha katika shule za chekechea jimboni Marsabit.

Kadhalika alidokeza kuwa mpango wa lishe shuleni unaendelea huku akiweka bayana kuwa wanatarajia unga wa uji utasambazwa katika shule zote za chekechea kufikia wiki ijayo kwa ajili ya muhula huu wa pili.

Subscribe to eNewsletter