Local Bulletins

IDARA YA AFYA KAUNTI YA MARSABIT KUAANZA KUWAFANYIA UCHUNGUZI WA HOMA YA NYANI YA MPOX WASAFIRI WOTE WANAOINGIA JIMBONI…

Na Caroline Waforo.

Idara ya afya kaunti ya Marsabit itaanza kuwafanyia uchunguzi wa homa ya nyani ya MPOX wasafiri wote wanaoingia jimboni.

Hii ni kutokana na kuendelea kurekodiwa kwa ugonjwa huo wa MPOX humu nchini pamoja na kisa kinachoendelea kufanyia uchunguzi katika kaunti jirani ya Isiolo.

Kulingana na afisa wa afya ya umma kaunti ya Marsabit Rob Golicha ni kuwa uchunguzi huo utaanza hivi karibuni ili kuwakinga wakaazi wa jimbo hili kutokana na ugonjwa huo.

Golicha anasema kuwa wanao maafisa nyanjani wanaoendelea kufanya ukaguzi wa MPOX katika maeneobunge yote manne ya kaunti ya Marsabit.

Kadhalika amewataka wakaazi jimboni Marsabit kutembelea kituo cha afya iwapo watapata dalili zozote zinazoambatana na mpox huku pia akitoa wito kwa washikadau mbalimbali kushirikiana na idara ya afya hata kwa kutoa hamasisho kwa umma.

Dalili za homa ya mpox mara nyingi hujitokeza siku 21 baada ya mtu kupata virusi hivyo.

Golicha anasema dalili kuu ya Mpox ni pamoja na kujikunakuna mwili, maumivu ya kifua, kuumwa na kichwa, homa, kupata vipele mwilini na kufura sehemu ya shingo kati ya nyingine.

Kwa hivi sasa taifa limerekodi visa vine katika kaunti za Taita Taveta, Busia, Nairobi pamoja na Nakuru.

Subscribe to eNewsletter