Local Bulletins

MOTO LAISAMIS WATEKETEZA SEHEMU KUBWA YA HIFADHI YA MELAKO

Picha. Hisani.

By Adano Sharamo

Sehemu kubwa ya hifadhi ya Melako eneo bunge la Laisamis imeteketea.
Kulingana na Afisa Mkuu wa hifadhi ya Melako Satim Eydmole, moto huo ulizuka Jumanne saa nane na kusambaa kwa kasi kwa sababu ya upepo.

Akizungumza kwa njia ya kipekee na Radio Jangwani kutoka eneo la mkasa, Eydmole ametoa wito wa ushirikiano kutoka maafisa wa hifadhi ya misitu nchini KFS, serikali ya kaunti na viongozi, kuzima moto huo unaoendelea kuteketeza kwa kasi sehemu ya hifadhi hiyo kati ya Loglogo na Laisamis.

Amesema wanakadiria kwamba moto huo ulioenea maeneo mbali tayari umekwisha teketeza zaidi ya kilomita 35 ya malisho.

Eydmole amesema wanakosa vifaa muhimu vya kudhibiti moto huo na hali mbovu ya barabara eneo hilo imefanya vigumu kufikisha msaada akibaini kuwa moto huo unahatarisha maisha ya viumbepori wa Malako.

Amesema msaada wa kipekee kufikia sasa wamepata kutoka kwa wakfu wa NRT na wananchi wanaendelea na juhudi za kuzima moto huo.

Wananchi wametakiwa kuwa waangalifu kwani moto huo unaweza kusambaa zaidi

Subscribe to eNewsletter