Local Bulletins

Mikahawa na mahoteli kufunguliwa japo kwa masharti wakati makali ya corona yakiendelea

Dr Rashid Amamn CAS wizara ya afya. Picha MOH.

Wamiliki wa mahoteli sasa wanahitajika kutuma maombi upya kabla ya kurejelea kazi zao. Hili ni agizo jipya kutoka serikali siku moja tu baada ya kutangaza kwamba wamiliki wa mikahawa mbali mbali wanaweza kurejelea kazi zao.

Kaimu mkurugenzi katika afya umma nchini Dkt Francis Kuria amesema kwamba wamiliki wa mahoteli wanahitajika kujaza fomu ambazo watazipakua kutoka wavuti wa wizara ya afya.

 Kisha fomu wameagizwa kuziwasilisha kwa maafisa wa afya ya umma katika kila kaunti na kusubiri ukaguzi kufanyika upya kabla ya kuanza kufanya kazi zao.

Dkt Kuria amesema kwamba katika fomu hiyo maafisa wa afya ya umma watahitajika kufanya ukaguzi na kuhakikisha usafi wa hali ya juu na maagizo ya serikali yanazingatiwa kabla ya mahoteli kuanza kutoa huduma zake tena.

 Wamiliki wa mahoteli watahitajika kuhakikisha kuwa wahudumu wote katika hoteli husika wamefanyiwa vipimo vya afya kuhakikisha kuwa wana leseni za afya, kuwa na vitakasa, maji yanayotiririka na sabuni na nafasi kubwa ya kutosha watu kukaa umbali wa mita moja nusu.

Wafanyibiashara wa mikahawa kadhaa hapa mjini marsabit wameonekena kurejelea kazi zao, licha ya wengi wao  kushindwa kutimiza baadhi ya masharti kama vile  kupimwa virusi vya korona kabla ya kufungua kazi zao kama ilivyotakiwa na wizara ya afya.

Wafanyibiashara hao wamesema kuwa wamelazimika kufungua biashara zao licha ya kushindwa kutimiza baadhi ya masharti kama vile  kupimwa virusi vya korona kabla ya kufungua kazi zao.

Wamelalamikia gharama ya juu ya zoezi hilo huku wakitaka serekali kusimamia gharama hiyo.

Aidha wengine wao wamelalamikia muda mfupi wa kufungua na kufunga biashara hizo huku wakiitaka  serekali kulegeza kamba na kuongeza saa za kuhudumu.

Kulingana nao ni kuwa wamelazimika kupunguza idadi ya wafanyikazi wao tangu virusi vya korona  kuadhiri taifa hili kwa ajili ya biashara kudora na kupelekea wao kukosa fedha za kuwalipa mishahara.

Hata hivyo wengine wao wameahidi kuwarejesha baadhi ya wafanyikazi wao kazini iwapo baishara zitaimarika.

Wengine wao wamesalia kufunga biashara zao, huku wakidai kuwa bado hali hayajaimarika  hapa nchini, na kuhofia kuwa virusi vya korona ambavyo tayari vimeripotiwa katika kaunti ya mandera huenda  vikasambaa zaidi na kuhatarisha maisha ya wakaazi wa ukanda huu wa kaskazini magharibi.

Wametaja kuwa bado serekali haijaweka mikakati kabambe ya kuzuia kusambaa kwa virusi hivyo hapa Marsabit na kupelekea kuhatarisha zaidi maisha yao.

Additional story by Machuki Dennson

 

Subscribe to eNewsletter