Highlights

Polisi wa Marsabit Central wanasa mafuta ya kupikia yanayoshukiwa kuingizwa nchini kinyume cha sheria.

Na Nyabande Orwa

Polisi wa Marsabit Central wamenasa mitungi 180 ya mafuta ya kupikia yaliyokuwa yakisafirishwa kutoka Somalia kuingia nchini kinyume cha sheria.

Akithibitisha tukio hilo, Kamanda wa polisi wa kaunti ya Marsabit, Leonard Kimaiyo, amesema mafuta hayo yalikamatwa leo yakisafirishwa kwa gari la abiria katika eneo la KBC, mjini Marsabit.

Kimaiyo amesema maafisa wa Mamlaka ya ushuru (KRA) walifika eneo la tukio na kubaini kuwa mafuta hayo hayakuwa yamelipiwa ushuru unaohitajika.

Dereva wa gari hilo amekamatwa na anatarajiwa kufikishwa mahakamani kesho kujibu mashtaka yanayohusiana na tukio hilo.

Wakati huo huo, kamanda Kimaiyo amewataka wakazi wa Marsabit kuwa waangalifu wanaponunua mafuta ya kupikia, akisema bidhaa zisizokidhi viwango vinaweza kuhatarisha afya ya watumiaji.

Aidha, amewahimiza wananchi kuendelea kushirikiana na vyombo vya usalama kwa kutoa taarifa kuhusu shughuli zozote wanazozishuku.

Post Comment