Kituo cha uokozi wa waathiriwa wa gbv kujengwa hospitali ya Rufaa ya Isiolo.
Na Samuel Kosgei
Mamlaka ya kusimamia barabara kuu nchini KENHA kupitia mradi wa Horn of Africa Gateway Project kwa ushirikiano na serikali ya kaunti ya Isiolo, imefanya hafla ya uwekaji wa jiwe la msingi kwa ujenzi wa kituo cha uokozi kwa waathiriwa wa dhuluma za kijinsia GBV Rescue Centre katika Hospitali ya Rufaa na Mafunzo ya Isiolo.
Akizungumza wakati wa hafla hiyo, mhandisi Joash Ochieng amesema kuwa ujenzi wa kituo hicho unatarajiwa kukamilika ndani ya kipindi cha miezi sita, huku akieleza kuwa mradi huo utasaidia kuimarisha huduma kwa waathiriwa wa dhuluma za kijinsia katika eneo hilo.
Kwa upande wake, Waziri wa Afya kaunti ya Isiolo Luqman Ahmed amepongeza hatua hiyo akisema serikali ya kaunti imejitolea kuwasaidia waathiriwa wa GBV kwa kila njia ili kuhakikisha wanapata huduma bora na msaada unaohitajika.
Naye Afisa Mkuu katika idara ya afya kaunti ya Isiolo Mohamed Abdikadir ameunga mkono kauli hiyo huku akisifia mradi huo kwa kusema utakuwa na mchango mkubwa katika kulinda na kuhudumia waathiriwa wa dhuluma za kijinsia kaunti ya Isiolo.



Post Comment