County Updates, Diocese of Marsabit, Local Bulletins

Mwanamke Mmoja Auwawa Huku Mbuzi Wake 40 Wakiibwa Na Majangili Waliojihami Kwa Bunduki Katika Lokesheni Ya Jirime Eneo La Milima Mitatu Usiku Wa Kuamkia Leo.

Picha;Hisani

By Mark Dida,

Mwanamke mmoja ameuwawa huku mbuzi wake 40 wakiibwa na majangili waliojihami kwa bunduki katika lokesheni ya Jirime eneo la Milima Mitatu usiku wa kuamkia leo.

Kwa mujibu wa kamishina wa kaunti ndogo ya Sakuu Peter Mureira, uvamizi huo ulitekelezwa na idadi isiyojulikana ya majangili waliojihami mwendo wa saa saba usiku.

Mureira amesema kwa sasa maafisa wa polisi wanaendelea kufuata nyao za mbuzi walioibwa ili kukabili wahalifu hao.

Inaarifiwa marehemu alitoka nje kuona kinachaoendelea kwenye boma lake kabla ya kupigwa risasi na alidhibitishwa kuaga dunia punde baada ya kufikishwa katika hospitali ya rufaa ya Marsabit.

Mureira amekilaani kitendo hicho huku akieleza masikitiko yake kuhusu misururu ya mashambulizi ya kikabila yanayoshuhudiwa jimboni ambayo imepelekea vifo vya raia na uharibifu wa mali.

Aidha amesema maafisa wa usalama wanaendelea na uchunguzi ili kubaini kiini cha kisa hicho huku maafisa polisi wa kukabiliana na wizi wa mifugo ASTU wakihusishwa kwenye operesheni ya kutafuta mbuzi hao walioibwa.

Kisa hiki kilijiri saa chache tu baada ya washukiwa wanne kukamatwa na Kitengo cha kushika doria Mpakani (BPU) kwa kusambaza silaha, risasi kwa pande zinazopigana katika mpaka unaokumbwa na ugomvi wa Turbi-Sololo.

Wiki iliyopita, Waziri wa  usalama wa ndani Fred Matiang’i alisema serikali itazindua zoezi la kuwapokonya silaha wenyeji hapa Marsabit na kaunti zote jirani kama moja wapo ya juhudi za serikali kudumisha amani katika eneo hili zima.

Subscribe to eNewsletter