Local Bulletins

VIJANA WA MARSABIT GEN Z WATAFANYA MAANDAMANO YA AMANI KUKATAA SHERIA YA FEDHA INAYOPENDEKEZWA

NA LELO WARIO

Vijana katika kaunti ya Marsabit wameapa kujiunga na wenzao kote nchi kufanya maandamano ya Amani kulalamikia mswada tata wa fedha mwaka wa 2024.

Vijana hao kwenye barua waliomwandikia msimamizi wa polisi (OCS)  mjini Marsabit Edward Mabonga wamesema kuwa maandamano yao yatakuwa ya Amani na utulivu na amewataka maafisa wa polisi mjini Marsabit kuwapa usalama wa kutosha kama sheria inavyosema.

 

Akizungumza na meza yetu ya habari, John Gutano ambaye ni mmoja wa viongozi wa vijana  ameeleza kuwa maandamano hayo yatakuwa ya Amani na amewahimiza vijana katika sehemu mbalimbali kujiunga nao li kupinga mswada huo wa fedha ambao ameeleza kuwa itawakandamiza.

 Aidha John ameelezea baadhi ya masuala yanayochochea wao kupinga mswada huo wa fedha ikiwemo madai ya ushuru mpya uliowekwa kwenye matibabu ya ugonjwa wa saratani, kutolewa kwa mpango wa lishe shuleni kati ya madai mengine.

Wanasema kuwa, maandamano hayo ya Amani ni kuwashinikiza wabunge wao wote kuwataka kupinga mswada wa fedha 2024.

Vilevile John   amewaonya vijana dhidi ya  kusababisha vurugu katika  maandamano na kusema kuwa atakayedhubutu kuleta ugomvi atachukuliwa hatua.

Maandamano hayo pia yanatarajiwa kufanyika katika mji wa North Horr.

Subscribe to eNewsletter