Local Bulletins

Serikali ya Marsabit yashutumu Seneta Mohammed Chute kwa kusambaza madai ya urongo

Na Samuel Kosgei

Serikali ya kaunti ya Marsabit imepinga madai kuwa ilihonga kamati ya Seneti kuhusu hesabu za umma ili kusitisha uchunguzi dhidi ya madai ya  ubadhirifu wa pesa za umma zilizotengewa serikali ya kaunti mwaka wa 2020/21.

Akizungumzia suala Hilo msemaji wa serikali ya kaunti ya Marsabiti Abdub Barille amemshutumu seneta wa Marsabit Mohammed Chute kwa kudai kuwa serikali ya Marsabit ilitoa hongo kwa maseneta ili kutupilia mbali uchunguzi dhidi ya gavana Mohamud Ali.

Barille akizungumza na wanahabari ofisini mwake amemtaka seneta Chute kuomba msamaha kutokana na kutoa madai asiyoweza kudhibitisha.

“Tunataka seneta aombe msamaha serikali ya kaunti Marsabit na gavana Mohamud Ali kwa madai kwamba sisi tulihonga kamati ya seneti” alisema Barille

Seneta Chute kupitia kituo kimoja cha radio na mitandao ya kijamii alidai kuwa maseneta hao walipewa shilingi milioni 12 ili uchunguzi dhidi ya gavana kuzimwa.

Barille Sasa anaitaka idara za uchunguzi nchini ikiongozwa na EACC kumwita seneta Chute ili aweze kuweka wazi madai yake au hata afike mbele ya kamati hiyo ya Seneti aweke wazi madai yake.

Subscribe to eNewsletter