Local Bulletins

Wenyeji wa Moyale waitaka serikali ya Kenya kufanya mazungumzo ya kibiashara na Ethiopia kulainisha hali

Na Winnie Adelaide

Kule moyale Wafanyibiashara wameitaka serikali kushughulikia kwa haraka mzozo wa mpaka wa Kenya na Ethiopia ili kuwaruhusu kununua bidhaa bila vizingiti kwa kuvuka Ethiopia.

Akizungumza na radio jangwani mwenyekiti wa Chama cha Wanabiashara na Viwanda mjini Moyale Mohammed Ali amesema kwamba serikali ya Kenya inafaa kuzungumza na mamlaka ya taifa la Ethiopia ili kuruhusu wafanyibiashara wa Kenya kununua bidhaa nchini humo kama vile mafuta.

Ali amesema kwamba serikali inafaa kuhakikisha kwamba wananchi wanaruhusiwa kufanya biashara kutoka pande zote mbili.

Ameongeza kuwa wafanyibiashara wamekuwa wakikamatwa na magari yao kuzuiliwa kwa madai kwamba wananunua mafuta kutoka taifa  jirani la Ethiopia.

Kauli yake Ali imeungwa mkono na Wakaazi wa Moyale wanaolalamikia ugumu wa Maisha kutokana na ongezeko la bidhaa muhimu kufuatia kuongezwa kwa bei ya mafuta nchini.

Lita moja ya petroli Moyale sasa ni Sh210 na dizeli Sh193, huku kilomita tano kuvuka mpaka, mafuta yanauzwa kwa Sh120 na Sh100 mtawalia.

Mjini Marsabit, lita moja ya petroli inagharimu Sh186 huku dizeli ikiuzwa Sh172.

Kwa sasa nauli ya basi kutoka Nairobi hadi Moyale, umbali wa kilomita 850, imepanda kutoka Sh3,000 hadi Sh5,000.

Matarajio ya wakaazi wengi Marsabit yanazidi kudidimia baada ya kupanda kwa bei ya mafuta huku wakiwa na wasiwasi kuwa huenda ongezeko hilo litachangia kupanda kwa bei za bidhaa muhimu.

Wakizungumza na shajara ya Radio Jangwani mjini Marsabit wakaazi tuliopata kuzungumza nao wametaja kuwa hali kwa sasa ni ya kusikitisha tangia kupanda maradufu kwa bei ya mafuta ya petroli huku gharama za bidhaa kadha wa kadha zikitarajiwa kuongezeka,wameeleza kuwa mfumko wa bei za bidhaa huenda ukawa donda sugu huku ukame ukizidi kuwatia wakaazi kiwewe.

Subscribe to eNewsletter