Highlights

Kituo cha Kitaifa cha Kupambana na Ugaidi (NCTC) kimetoa wito kwa viongozi Marsabit kuepuka kuchochea migogoro inayoweza kutumiwa na makundi ya kigaidi.

Na Silvio Nangori

Viongozi katika Kaunti ya Marsabit wametakiwa kujiepusha na kutumia wananchi katika kuchochea au kuendeleza fujo, kwa kuwa hali hiyo inaweza kutumiwa kama njia ya kupenyeza kwa makundi ya kigaidi.

Wito huo umetolewa na Afisa wa Mahusiano katika Kituo cha Kitaifa cha Kupambana na Ugaidi (NCTC), Joseph Kanyiri, ambaye ameonya kuwa makundi hayo hutafuta mianya ya kuingia katika jamii kwa lengo la kutekeleza uhalifu na hata kuwashawishi vijana kujiunga na shughuli zao.

Kanyiri amesema kuwa migogoro ya kijamii inapochochewa, inatoa nafasi kwa makundi hayo kueneza ushawishi wao, hivyo akasisitiza umuhimu wa viongozi kuwa na busara katika kauli na matendo yao ili kulinda amani kaunti ya Marsabit

Amezitaka jamii za Marsabit kushirikisha wazee na viongozi wa mila katika kutatua changamoto na migogoro inayoibuka, akisema kuwa mbinu hiyo itasaidia kuzuia kuongezeka kwa mizozo ambayo inaweza kuwa tishio kwa usalama Marsabit.

Aidha, amewahimiza viongozi wa dini kuongeza juhudi katika kueneza ujumbe wa amani, umoja na utangamano, pamoja na kuwahimiza vijana kujiepusha na kushiriki katika shughuli zinazoweza kuhusishwa na ugaidi.

Kanyiri amesisitiza kuwa ushirikiano wa karibu kati ya jamii, viongozi wa dini na serikali ni muhimu katika kudhibiti vitendo vinavyoweza kuhatarisha usalama wa Marsabit na maeneo jirani.

Post Comment