Local Bulletins

Zaidi ya 80% ya watu wa Marsabit wanahitaji msaada wa dharura asema gavana Mohamud Ali

Na Samuel Kosgei

Gavana wa Marsabit Mohamud Ali ameomba mashirika ya kibinafsi kuendeleza kwa miezi sita zaidi miradi ya kusaidia familia zinazokumbwa na athari za ukame Jimboni kipindi hiki cha ukame.

Akizungumza alipopatana na washikadau wanaohusika na mikakati ya kupambana na majanga Jimboni (CSG) gavana Ali amekiri kuwa hali ya Wananchi wanaohitaji msaada wa kiutu inazidi kuwa mbaya hivyo mikakati mwafaka inahitajika ili kuokoa binadamu na mifugo.

Gavana Abshiro anasema kuwa asilimia 80 ya wananchi Marsabit wanahitaji msaada wa chakula na hivyo kabla ya bajeti ya kaunti kuidhinishwa na bunge anasema kuwa kufikia mwisho wa wiki hii kiasi fulani ya chakula kitatolewa kwa wananchi huku wakisubiri bajeti kupitishwa.

Wakati uo huo waziri wa fedha kaunti hii Malicha Boru amekana madai yanayosambaa mitandaoni kuwa fedha zaidi ya million 700 iliyopitishwa mwaka Jana na wawakilishi wadi ilifujwa bila kusaidia watu.

Malicha amesema kuwa pesa hizo zilitumika kwa awamu Tatu. Mwezi October – November shillingi million 210 zilitumika kununua Michele, maharagwe, mafuta ya kupika na Mahindi.

Mwezi January – Machi mwaka huu shillingi millioni 259 zilitumika huku zilizosalia zikitumika katika mwezi wa tano na mwezi Juni mwaka huu.

Wakati uo huo ameitaka Bunge la kaunti kupitisha bajeti ya sasa ili millioni 700 zilizotengwa kwenye bajeti zitumike kusaidia na kuokoa maisha

Idara zote za dharura ikiwemo zile za maji, mifugo, elimu na afya zimewasilisha mahitaji Yao ya dharura kwa kamati maalum ya kitaifa inayokusanya ripoti kamili kabla ya kuiwasilisha Hadi ofisi ya naibu wa Rais siku ya Jumatano.

Kwa upande wake serikali kuu kupitia kamishna wa kaunti ya Paul Rotich amesema kuwa hivi karibuni serikali itakuwa inakumbatia kuwapa watu pesa badala ya kuwapa chakula kutokana na gharama ya kusafirisha chakula hicho.

Kamati ya kiufundi ya dharura imeafiki kufanya mkutano kila wiki ili kutathmini hali huku mkutano wa washikadau wote ukipangwa kufanyika mara mbili kila mwezi.

Washikadau aidha wameitaka serikali kuu na ile kaunti kusimamisha miradi nyingine za maendeleo na kuelekeza fedha nyingi kwenye suala la athari za ukame

Subscribe to eNewsletter