Maafisa wa polisi Marsabit kutumia mahakama tamba kuwawajibisha madereva wanaokiuka sheria za trafiki papo hapo.
NA NYABANDE ORWA
Kamanda wa Polisi wa kaunti ya Marsabit, Leonard Kimaiyo, ametoa wito kwa madereva kuwa waangalifu katika msimu huu wa sherehe za krismasi na mwaka Mpya ili kupunguza ajali za barabarani.
Akizungumza na kituo hiki, Kimaiyo amesema kuwa maafisa wa polisi wameimarisha doria katika barabara kuu ya Isiolo–Marsabit ili kudhibiti madereva wanaokiuka sheria za trafiki. Ameongeza kuwa polisi wameshirikiana na idara ya mahakama kuweka mahakama tamba barabarani ili kuwawajibisha madereva wanaopatikana na makosa ya trafiki papo hapo.
Kamanda huyo amewataka madereva kuepuka matumizi ya pombe na dawa za kulevya wanapokuwa barabarani, kupumzika vya kutosha na kuhakikisha magari yao yako katika hali nzuri kabla ya kuanza safari.
Kauli ya kamanda huyo imekuja wakati ambapo visa vya ajali za barabarani vinaendelea kuongezeka. Kulingana na mamlaka ya usalama barabarani, NTSA, watu 4,458 wamefariki dunia kutokana na ajali za barabarani nchini hadi kufikia tarehe 2 Desemba mwaka huu, huku idadi hiyo ikiendelea kuongezeka kutokana na ajali mpya zinazorekodiwa kila siku.



Post Comment