Local Bulletins

Washukiwa wa mauaji ya Polisi wazuiliwa rumande kwa wiki mbili Zaidi Marsabit

Na Grace Gumato

Washukiwa wa mauaji ya afisa wa polisi kule Qubi Qalo watazuiliwa kizimbani kwa siku kumi na nne kuruhusu uchunguzi kukamilika kabla ya kesi yao kurejelewa tena tarehe 31 mwezi huu. Hii ni baada ya mahakama ya hapa Marsabit kuupa upande wa mashtaka muda huo washukiwa walipowasilishwa mbele yake jana Jumatatu.

Washukiwa hao Roba Jarso na Galgallo Boru -wote raia wa Ethiopia pamoja na mkenya Roba Sora walifikishwa katika mahakama ya Marsabit wakikabiliwa na mashtaka pia ya kumua afande Kenedy Leyan na kumjeruhi mwenzake. Aidha wanadaiwa kumuua raia mmoja kwa jina Dadach Galgallo-mkazi wa Qubi Qallo. Washukiwa wanakabiliwa na kosa jingine la kupatikana na bunduki kinyume na sheria.

Afisa huyo wa polisi aliyeuawa alipigwa risasi na wezi wa mifugo katika eneo la Kubi Qallo wiki mbili zilizopita katika tukio ambapo pia afisa mwingine wa polisi aliponea kwa jeraha baada ya kupigwa risasi na wezi wa mifugo wakati walipokuwa wakisaka mifugo iliyokuwa imeibiwa siku za awali.

Washukiwa hao watatu walikamatwa wikendi ambapo polisi pia walifanikiwa kupata bunduki mbili na risasi kutoka kwa watatu hao katika operesheni kali katika eneo la Goro-Rukesa, hapa Saku.

Kulingana na naibu kamishna wa Marsabit central David Saruni, kikosi cha maafisa wa polisi kilitumwa eneo hilo kufuatia taarifa ya kijasusi, ambapo bunduki aina ya AK 47 na bunduki aina ya SHE, magazine mbili na risasi 13 zilipatikana.

Saruni ameongeza kuwa washukiwa hao walionekana wakiwa wamejificha msituni na wananchi ambao walitoa taarifa kwa mamlaka ambayo ilichukua hatua mara moja.

 

Subscribe to eNewsletter