Highlights

Serikali na wadau mbalimbali watakiwa kufanya mazungumzo ya kina kuhusu changamoto zinazoikabili elimu na vijana

Na JB Nateleng

Askofu wa Jimbo Katoliki la Marsabit, Mhashamu Peter Kihara, ametoa wito kwa serikali na washikadau mbalimbali nchini kuanzisha mazungumzo ya kitaifa ili kutafuta suluhu ya changamoto zinazowakabili vijana na taifa kwa ujumla.

Askofu Kihara amesema kuna ongezeko la sintofahamu kati ya vijana na viongozi, kutokana na kupungua kwa imani ya vijana kwa viongozi wao akisema hali hiyo inachangiwa na ukosefu wa ajira pamoja na kudorora kwa ubora wa elimu, ambayo ni msingi muhimu wa maendeleo ya jamii.

Aidha, ameonya kuwa bila hatua za haraka, pengo kati ya vijana na viongozi litaendelea kuongezeka.

Kwa upande wake, Mkurugenzi wa Elimu katika Jimbo Katoliki la Marsabit, Padri Abraham Ali, amesema shule nyingi jimboni bado hazina mazingira bora ya kufunzia akilaumu serikali na viongozi kwa kushindwa kuwekeza vya kutosha katika miundombinu ya elimu.

Naye mkurugenzi wa elimu wa Kaunti ya Marsabit William Kamugunah, amewataka wazazi kushiriki kikamilifu katika masuala ya elimu kwa kuwapeleka watoto shule na kuunga mkono maendeleo ya taasisi za elimu.

Kamugunah pia ameitaka jamii kuachana na mila potovu zinazowazuia watoto kupata elimu, akisisitiza kuwa kila mtoto ana haki ya kusoma.

Post Comment