Mwalimu akamatwa kwa tuhuma za kumnajisi na kumpachika mimba mwanafunzi wake wa gredi saba, Kargi
Na Caroline Waforo
Mwalimu mmoja wa shule ya msingi ya Mission of Hope International iliyoko Kargi kaunti ndogo ya Loiyangalani kaunti ya Marsabit amekamatwa kwa tuhuma za kumnajisi na kumpachika mimba mwananfunzi wake wa gredi ya saba aliye na umri wa miaka 14.
Akithibitisha kisa hicho OCPD wa Loiyangalani Nicholas Mutua amesema kuwa uchunguzi unaashiria kuwa mwaathiriwa ana ujauzito wa miezi mitatu.
Aidha, Mutua amesema kuwa madai yameibuka kuwa si mara ya kwanza kwa mshukiwa kuhusishwa na visa vya aina hiyo, huku akidaiwa kuwapachika mimba wanafunzi wengine wanne katika eneo la Kargi.
Amesema kuwa mwalimu huyo tayari amekamatwa huku uchunguzi ukiendelea ili kubaini ukweli wa madai hayo na hatua zaidi za kisheria kuchukuliwa
OCPD Mutua amesema kuwa vipimo vya msimbojeni DNA vitafanyika kusaidia katika uchunguzi huo.
Aidha amewataka wananchi kushirikiana kwa karibu na vyombo vya usalama kwa kuripoti visa vya dhuluma dhidi ya watoto mapema ili hatua zichukuliwe haraka.
Vilevile OCPD Mutua ametoa onyo kali kwa wanaojihusisha na vitendo vya unyanyasaji wa kingono dhidi ya watoto akisema watachukuliwa hatua kali za kisheri.



Post Comment