Kesi Dhidi ya kampuni ya BP inayodaiwa kufanya Uchafuzi wa Mazingira Kargi na Kalacha kuanza kutajwa Mahakamani Isiolo siku ya Jumatano
Mahakama ya Mazingira na Ardhi imeamua kuwa kesi ya pamoja dhidi ya kampuni ya mafuta ya BP plc itaendelea kusikilizwa. Kesi hiyo itatajwa tarehe 6 mwezi huu kwa ajili ya maelekezo, hatua ambayo mahakama itaweka mwongozo wa jinsi usikilizaji kamili utakavyoendeshwa.
Mnamo Februari mwaka huu jumla ya walalamishi 299 waliwasilisha kesi katika Mahakama ya Mazingira na Ardhi mjini Isiolo wakidai kuwa kampuni ya BP ilisababisha uchafuzi mkubwa wa mazingira kupitia utupaji usiofaa wa taka hatari zilizotokana na shughuli za utafiti wa mafuta kaskazini mwa Kenya.
Kulingana na maombi yao, shughuli za utafiti zilizofanywa miaka ya 1980 na kampuni ya Amoco Corporation – iliyokuja kununuliwa na kampuni ya BP mwaka 1998 – zilihusisha uchimbaji wa visima kadhaa visivyokuwa na mafuta karibu na maeneo ya Kargi na Kalacha katika Jangwa la Chalbi.
Walalamishi wanadai kuwa taka zenye sumu na mionzi kutoka shughuli hizo zilitupwa ovyo katika mazingira, hali iliyochafua maji ya ardhini na kusababisha maradhi pamoja na vifo vya mamia ya wakazi na mifugo katika jamii zinazozunguka maeneo hayo.
Mlalamishi mkuu ni aliyekuwa mwakilishi wadi wa Kargi Assunta Galgidele na watu wengi 298.



Post Comment