Kanisa Katoliki laendelea kukuza elimu maadili na nidhamu miongoni mwa wanafunzi Marsabit asema Padri Abraham Ali.
Na JB Nateleng
Kanisa Katoliki limeendelea kutoa mchango mkubwa katika jimbo la Marsabit, hasa katika kukuza elimu, maadili na nidhamu miongoni mwa wanafunzi.
Kwa mujibu wa Mkurugenzi wa Elimu katika Jimbo Katoliki la Marsabit, Padri Abraham Ali kanisa bado ni nguzo muhimu katika sekta ya elimu. Amewahimiza wazazi kufuata mfano wa wamisionari wa awali waliowasili eneo hili na kujitolea kuelimisha jamii kuhusu dini na maisha ya familia.
Akizungumza na idhaa hii katika ofisi yake, Padri Abraham amesisitiza umuhimu wa ushirikiano kati ya serikali, wadau wa elimu na wazazi ili kuboresha na kuinua viwango vya elimu katika kaunti ya Marsabit.
Padri Abraham ameongeza kuwa kwa sasa Kanisa Katoliki linamiliki takriban nusu ya shule za msingi na sekondari katika jimboni jambo ambalo amesema linachangia kwa kiasi kikubwa upatikanaji wa elimu bora kwa wanafunzi.
Aidha amewakaribisha waumini, walimu na wanafunzi kushiriki katika maadhimisho ya siku ya elimu itakayofanyika katika Parokia ya Loiyangalani, Jumamosi tarehe 16 Mei 2026.



Post Comment