Idara ya watoto Marsabit yafafanua uamuzi wa Mahakama kuwa wasishtakiwe wavulana wanaoshiriki mapenzi na wasichana kwa maelewano
Na JB Nateleng
Afisa wa masuala ya watoto katika kaunti ndogo ya Marsabit Central, Leakey Mukanzi, amesema uamuzi wa Mahakama Kuu kwamba wasishtakiwe wavulana walio chini ya umri wa miaka 18 wanaoshiriki mapenzi na wasichana wa umri sawa kwa maelewano, ulilenga kuondoa sheria iliyokuwa ikionekana kumkandamiza mtoto wa kiume.
Akizungumza afisini mwake, Mukanzi amefafanua kuwa uamuzi huo haukuhalalishi mahusiano ya kimapenzi miongoni mwa watoto walio chini ya umri wa miaka 18 akisisitiza kuwa bado si jambo linalofaa kwa matineja kujihusisha na masuala ya mapenzi.
Amesema hatua hiyo pia inalenga kutoa nafasi kwa maafisa wa watoto, wazazi na walimu kuwashauri na kuwapa mawaidha vijana wanaojihusisha na mapenzi katika umri mdogo.
Mukanzi pia amesisitiza umuhimu wa wazazi kuwa karibu na watoto wao kwa kufahamu walipo na shughuli wanazofanya ili kusaidia kupunguza visa vya watoto kupotea kutokana na utepetevu wa malezi.
Aidha, amewataka wazazi na jamii kushirikiana katika kuwaongoza watoto kuhusu maadili mema na umuhimu wa elimu kwa ajili ya kujenga jamii bora kwa vizazi vijavyo.



Post Comment