Serikali yaondoa rasmi kesi ya ugaidi dhidi ya wazee wawili wa jamii wa Borana
Serikali imeondoa rasmi kesi inayofungamana na ugaidi dhidi ya aliyekuwa chifu wa Sololo Dabasso Dambi pamoja na mzee Guracha Dambala katika mahakama ya Kahawa.
Hatua hiyo inahitimisha rasmi mchakato wa kesi iliyokuwa ikiwakabili.
Haya yanajiri saa chache baada ya wawili hao kuachiliwa huru usiku wa jana Jumatatu kwa bondi ya shilingi milioni 5 baada ya kuzuiliwa katika gereza la Kamiti.
Wakizungumza baada ya uhuru huo wawili hao walishukuru na kupongeza viongozi wa kaunti ya Marsabit pamoja na wananchi kwa kusimama nao kipindi chote walichokamatwa na kuzuiliwa.
Itakumbukwa kuwa kukamatwa kwa wawili hao kulihusishwa na mzozo wa ardhi uliokuwa ukiendelea kati ya kaunti za Marsabit na Wajir.
Maandamano yalishuhudiwa katika miji ya Moyale, Marsabit na Sololo kupinga ujenzi wa kituo cha usalama katika eneo lililokuwa likizozaniwa la Basir.
Baadaye, serikali kupitia wizara ya usalama wa ndani iliamuru kusitishwa kwa mradi huo na kuwaagiza Makamishna wa Mikoa ya Kaskazini Mashariki na Mashariki kutambua eneo jipya litakalokubalika kwa pande zote kwa ajili ya ujenzi wa kituo hicho cha usalama wa mashirika mbalimbali.



Post Comment