Viwango vya matumizi ya dawa za kulevya vimeripotiwa kuwa juu, Marsabit
NA Caroline Waforo
Viwango vya matumizi ya dawa za kulevya katika kaunti ya Marsabit vimeripotiwa kuwa juu.
Kwa mujibu wa Mratibu wa Mamlaka ya Kitaifa ya Kupambana na Matumizi ya Dawa za Kulevya na Mihadarati (NACADA) tawi la Marsabit, Mohammed Waqo, hali hiyo inachangiwa na mpaka wa Kenya na Ethiopia unaoendelea kutumika katika ulanguzi wa dawa hizo.
Haya yamebainika huku mamlaka hiyo ya NACADA ikiendelea na kampeni ya siku tano ya kuhamasisha wananchi dhidi ya matumizi dawa za kulevya na pombe haramu.
Na kama njia moja ya kukomesha uuzaji wa pombe haramu jimboni Marsabit, Waqo amesema kuwa mamlaka ya NACADA imeanza kuwawezesha kina mama wanaojihusisha na biashara hiyo haramu ili wajihusishe na shughuli mbadala za kujitafutia mapato.
Vilevile wazazi wametakiwa kuwajibika katika malezi ya watoto wao ili kuwaepusha na matumizi ya dawa za kulevya pamoja na pombe haramu.
Aidha wadau mbalimbali katika jamii wametakiwa kushirikiana kikamilifu katika juhudi za kukabiliana na matumizi ya vileo hasa miongoni mwa vijana.
Kampeni hiyo iliyong’oa nanga siku ya Jumatatu itakamilika siku ya Ijumaa, ikilenga makundi mbalimbali ikiwemo wanafunzi na wafanyabiashara wa vileo miongoni mwa wengine.



Post Comment