Walimu wapya 84 waajiriwa na serikali ya jimbo ili kuinua viwango vya elimu ya ECDE
NA JB Nateleng
Idara ya Elimu ya Chekechea katika Kaunti ya Marsabit imeajiri walimu 84, kama sehemu ya juhudi za kuboresha na kuimarisha elimu ya awali kwa watoto.
Walimu hao kwa sasa wanapokea mafunzo elekezi yatakayowawezesha kuelewa majukumu yao na kutoa malezi na mafunzo bora pamoja na mazingira salama kwa wanafunzi katika shule zote za ECDE watakazopangiwa.
Walimu hao wametoka katika kaunti ndogo zote za Marsabit na wanatarajiwa kusambazwa katika shule mbalimbali za chekechea kote jimboni kulingana na mahitaji.
Akizungumza wakati wa mafunzo hayo, Waziri wa Elimu wa Kaunti ya Marsabit, Ambaro Abdullah Ali, amesema ajira hiyo imewezekana baada ya serikali ya kaunti kutenga fedha za kutosha kusaidia shughuli za idara yake.
Amewahimiza walimu hao kufanya kazi kwa bidii, uadilifu na kujituma ili kuinua hadhi ya elimu ya chekechea pamoja na kuhudumia watoto na jamii ipasavyo.
Aidha, waziri huyo amesema serikali ya kaunti imeendelea kuboresha miundombinu ya elimu ya ECDE kwa kujenga madarasa 202, vyoo 201, majiko ya kisasa 89 na kusambaza matanki 102 ya maji katika shule mbalimbali.
Vilevile, ameongeza kuwa serikali imesambaza uji katika shule zote za chekechea jimboni, hatua ambayo amesema imechangia kuongeza mahudhurio na kuwafanya watoto kubaki shuleni.



Post Comment