Madaktari Marsabit waafikiana na serikali ya kaunti kurejea kazini.
NA NYABANDE ORWA
Ni afueni kwa wagonjwa katika kaunti ya Marsabit baada ya madaktari kusitisha mgomo wao uliodumu takriban siku 13.
Akizungumza kwa njia ya simu na kituo hiki, Afisa wa uhusiano mwema wa chama cha madaktari KMPDU tawi la Marsabit, Dkt. Isaac Karogo, amesema walikubali kurejea kazini Jumatano baada ya mazungumzo yao na serikali ya kaunti kuzaa matunda.
Dkt. Karogo anasema walikubaliana kuunda kamati itakayowakilisha pande zote mbili,serikali ya kaunti na uongozi wa KMPDU. Kamati hiyo imepewa wiki mbili kushughulikia masuala yanayoweza kutatuliwa haraka, na mwezi mmoja kwa yale yanayohitaji muda zaidi.
Amesema pia tayari serikali ya kaunti imelipa madaktari malimbikizi ya mishahara hadi mwezi Oktoba. Hata hivyo, masuala ya bima ya afya, kupandishwa vyeo na makato ya kila mwezi bado yanafanyiwa mipango kabla ya kutekelezwa kikamilifu.



Post Comment