County Updates, Diocese of Marsabit

Shughuli Ya Kuwaajiri Makurutu Wa Polisi Imefanyika Jana Katika Vituo Mbali Mbali Kote Nchini.

 

Afisa Mkuu wa zoezi Kipkemoi Kulei. Picha Jillo Dida

 

By Jillo Dida

Shughuli ya kuwaajiri makurutu wa polisi imefanyika jana katika vituo mbali mbali kote nchini.

Idadi ndogo ya vijana ilishuhudiwa katika vituo mbali mbali vya kaunti ndogo zote za Marsabit.

Zoezi hilo limefanyika katika maeneo tofauti katika kaunti ya Marsabit yakiwa ni pamoja na Laisamis, Loiyangalani, Marsabit Central, Dukana, Sololo, Turbi, Moyale na North Horr.

Akizungumza na waandishi wa habari baada ya kukamilika kwa zoezi la kusajili makurutu hao katika eneo bunge la Saku, Afisa Mkuu wa kusimamia shughuli hiyo Kipkemoi Kulei amesema kuwa idadi ndogo ya vijana waliojitokeza  imechangiwa na changamoto kadhaa kama vile baadhi ya vijana kukosa kutimiza masharti hitajika.

Takriban vijana 70 walijitokeza kushiriki zoezi hilo huku eneo bunge la Saku likitengewa nafasi 5 pekee. Vijana wawili kati yao walisajiliwa kwenye kitengo cha GSU, wengine wawili kwenye kitengo cha polisi wa kawaida na msichana mmoja akiteuliwa kujiunga na kitengo cha polisi wa utawala AP.

Hata hivyo Kipkemoi ameeleza kusikitishwa na idadi ndogo ya nafasi iliyotengewa eneo la Saku licha ya idadi kubwa ya watu wa makabila tofauti kuishi hapa mjini.

Serikali inawaajiri makurutu wa polisi wapatao 4,700 na makurutu 300 wakiwa polisi wataalamu.

Shughuli iliyoanza jana ni ya kuwaajiri makurutu wa kawaida ilhali wale watakaojiunga na polisi kama wataalamu wakisubiri kujua hatima ya maombi yao waliyoyatuma kwa tume ya huduma za polisi.

 

Subscribe to eNewsletter