County Updates, Local Bulletins

Ahirisha BBI mpaka 2023 Maaskofu wa Katoliki wasema

Maaskofu wa Kanisa katoliki wakiwahutubia wanahabari, awali. Picha Kenya Catholic Media Network.

Na Machuki Dennson

 

Kanisa Katoliki limetaka mchakato wa kubadilisha katiba kupitia BBI kuahirishwa hadi baada ya uchaguzi mkuu ujao wa mwaka 2022.

 

Katika ujumbe wao hii leo maaskofu wamewataka viongozi kuheshimu katiba na taasisi za kisheria.

 

Wamependekeza kuwa mabadiliko muhim,u na ya dharura yafanyike kupitioa miswada ya bunge ili kufanikisha uchaguzi ujao ambao wamesema haufai kuahirishwa kwa sababu yoyote ile.

 

Wakihutubu leo ikiwa siku yao ya mwisho ya mkutano wao wa wiki nzima, maaskofu wameikosoa serikali kwa kuchelewa muda wote kuwateua makanishna wapya wa tume huru ya uchaguzi na mipaka nchini IEBC.

 

Kanisa katoliki linashangaa ni kwa nini uteuzi wa makamishna hao haujafanyika miaka miwili tangu makamishna watatu wajiondoe.

 

Kwenye taarifa iliyosomwa na mwenyekiti mpya wa baraza la maaskofu wa kanisa katoliki nchini KCCB, Askofu mkuu wa jimbo kuu la Mombasa, Martin Kivuva Musonde, Maaskofu wameonyesha wasiwasi wao kufuatia hatua ya rais Uhuru Kenyataa kudinda kuwateua majaji 41 waliopendekezwa na tume ya huduma za majaji nchini.

 

Kanisa linasema hatua ya rais inaibua taharuki katika ya idara ya mahakama na tawi kuu la serikali. Tayari hatua hiyo imeathiri utendakazi wa mahakama.

 

Kanisa aidha limetoa wito kwa wakenya kurejelea katika njia za zamani na za kawaida katika kutatua malumbano ya kila mara.

 

Hii ni kufuatia visa vya mauaji ambayo vimeshuhudiwa kuongezeka katika siku za maajuzi.

Maaskofu wamerejelea visa ambapo miili ya watu imekuwa ikipatikana ndani ya misitu wakati wanaotekeleza mauaji hayo hawajulikani.

 

Wametoa wito kwa wakenya kurejelea mazungumzo na kumaliza ugomvi baina yao.

 

Vile vile wamegusia tahadhari ambayo imetolewa nchini na watabiri wa hali ya hewa kwamba muda mrefu wa kiangazi utashuhudiwa katika baadhi ya maeneo.

 

Wameitaka serikali kuweka mikakati ya haraka ili kukabiliana na baa la njaa ili kuokoa maisha.

 

Subscribe to eNewsletter