County Updates, Diocese of Marsabit, Local Bulletins

Wakaazi wa lokesheni ya Tigo eneo bunge la North Horr watoa wito kwa serikali kuwajengea shule ya msingi.

Na Samwel Kosgei,

wa lokesheni ya Tigo eneo bunge la North Horr kaunti ya Marsabit, wametoa wito kwa serikali kupitia viongozi wao kuwajengea shule ya msingi katika eneo hilo. Wakaazi hao kwa masikitiko wameambia Shajara Ya Jangwani kuwa ukosefu wa shule ya msingi ya umma umewaathiri wanafunzi wengi kwani baadhi yao husoma tu hadi shule ya chekechea na kuacha masomo kutokana na umbali wa shule ya msingi ya umma.

Akizungumza na kituo hiki katika eneo la Burgabo mwalimu wa shule ya chekechea Tume Harro amesema kuwa shule ya msingi ya umma iliyo karibu inapatikana katika eneo la Turbi ambayo ni zaidi ya kilomita 25 na ile ya Bubisa ambayo ni kilomita karibu 50 kutoka Tigo.

Hali hiyo anasema hukera kwa kuwa ni sharti mzazi awe na familia katika maeneo hayo au mtoto asome bweni suala linalohitaji mwanafunzi awe na umri ya kuweza kujihudumia bila mzazi.

Mwalimu huyo wa kujitolea kusomesha watoto zaidi ya 30 wa chekechea ametolea mfano mwanafunzi wa miaka minane Umuro Boya ambaye amerudia shule ya watoto wadogo mara mbili kwa kukosa shule ya kuenda.

Shule ya pekee ya msingi tigo ni shule ya kibinafsi ambayo mlezi wake hawezi kumudu karo.

Mzee wa manyatta hiyo ya Tigo Sharamo Sacko ameambia shajara kuwa ipo haja ya serikali ya kaunti na ya kitaifa kushirikiana ili kuwajengea shule na kuwaajiri walimu wa kutosha ili wanao kufaidi na elimu ambayo ni haki yao.

Aidha anasema kutokana na ukosefu huo wa shule ya msingi ya umma wengi wa watoto wanalazimika kuacha masomo na kuwa wachungaji wa mifugo huku wasichana wakiolewa katika umri mdogo.

Subscribe to eNewsletter