Local Bulletins

Ukeketaji na ndoa za mapema zatajwa kuongoza kati ya visa vya dhulma za kijinsia katika kaunti ya Marsabit.

Na Caroline Waforo,

Visa vya ukeketaji dhidi ya watoto wa kike pamoja na ndoa za utotoni vimetajwa kuongoza kati ya visa vya dhulma za kijinsia katika kaunti ya Marsabit.

Haya yamebaika katika kikao cha kukusanya maoni kuhusu ongezeko la visa vya dhulma za kijinsia na mauaji ya wanawake kilichoendeshwa na jopo maalum la kuchunguza visa hivi liloloteuliwa na Rais William Ruto miezi mitatu iliyopita kufuatia ongezeko la mauaji ya wanawake hapa nchini.

Kulingana na Michael Kariuki anayesimamia jopo linalokusanya maoni katika kaunti hii ya Marsabit, wengi wa wakaazi ambao wametoa maoni wamevitaja visa hivi huku wakitoa wito wa hatua madhubuti kuchukuliwa ukitolewa.

Kariuki anasema kuwa pana haja ya kuangazia upya sheria zilizopo ili kukabiliana na visa hivi na kuziba mwanya uliopo.

Kulingana na Kariuki wananchi pia wamependekeza kujengwa kwa makao salama jimboni ili kuwapa hifadhi waathiriwa wa dhulma za kijinsia.

Vile vile swala la usawa wa ugavi wa raslimali limeibuka katika kikao hicho huku Kariuki akisema kuwa wanawake wamelalama kutengwa.

Wakizungumza katika kikao hicho wanawake wamelalama kutengwa haswa kwenye uridhi wa ardhi hili likitokana na mila na tamaduni za jamii za hapa jimboni Marsabit.

Kamati hii inayoongozwa na aliyekuwa naibu jaji mkuu Nancy Barasa iliteuliwa na Rais William Ruto kutokana na ongezeko la visa vya mauaji dhidi ya wanawake.

Katika miezi tatu ya kwanza ya mwaka 2025 takriban wanawake 129 waliuawa nchini, huku karibu visa vyote vikiripotiwa kuwa mauaji. Hayo yanajiri wakati visa hivyo vikizidi kuongezeka.

Asilimia 60 ya visa hivyo inaonyesha kuwa waathiriwa waliuawa na jamaa zao wa karibu.

Subscribe to eNewsletter