Local Bulletins

Rais William Ruto ataka maombi wakati akifanya juhudi kubadili uchumi

Rais William Ruto hii leo ameandaa ibada ya shukran kwa mwenyezi Mungu kufuatia ushindi wao katika uchaguzi mkuu uliopita maajuzi.

 Ibada hiyo imefanyika katika ikulu ya rais Nairobi. Rais Ruto amewashukuru wake wote kwa uchaguzi uliokamilika akisema kuwa ushindi wake ni ushindi wa wote.

Rais amewataka wahubiri na wainjilisti kuombea maswala matatu kwa ajili ya uongozi wake.

Maswala hayo ni pamoja na mpango wa serikali ya UDA.

Mpango wa serikali ya UDA ukiwa ni kulisha kila  mkenya aliye na njaa, kila mkenya aliye na mzigo wa kulipia malipo ya hospitali na bima ya matibabu na vile vile mpango wa kuhakikisha wakenya wanapata makaazi ya heshima.

Ruto anataka maombi kwa ajili ya uchumi wa kenya. Anasema asilimia 65 ya ushuru wa kenya unaokusanywa unatumiwa kulipia madeni ya taifa na hivyo kuharibu Zaidi uchumi.

Rais anasema kwamba serikali yake ina mpango mzuri na ana matumaini ya mambo kunyooka. Amesema kuwa taifa la Kenya limekop Zaidi kwa sababu ya kutotumia mali yake vizuri na kuwaachia vizazi vijavyo madeni.

Katika hotuba yake rais amerejelea uamuzi wa mahakama mapema wiki hii kuhusu hazina ya uzeeni NSSF.

Katika uamuzi huo mahakama iliizuia serikali kuongeza na hata kutekeleza sera hiyo ikisema ni haramu na kwamba haijafuata sheria.

Kwa sasa nchini wale ambao wameajiriwa wanakatwa shilingi mia mbili pekee kama hazina ya uzeeni.

Rais anasema kwamba mchango wa shilingi mia mbili ni mdogo sana na kwamba mswada utarekebishwa na kuwasilishwa kwa mabunge yote mawili kwa ajili ya kupitishwa uwasaidie wakenya.

Rais Ruto amewataka wakenya kuombea amani akisema taifa hili linatazamwa ka kielelezo chema katika ukanda wa Afrika mashariki na ziwa kuu.

Rais amerejelea kisa cha juzi ambapo askari wanane waliuawa na majambazi katika kaunti ya Turkana ambapo amesema hilo litakuwa la mwisho. Ruto amesema kuwa sasa idara ya polisi inayo bajeti yake na sasa ni wakati waweze kuimarisha utendakazi wao kwa wakenya.

Ruto amewashukuru Spika wa bunge la kitaifa Moses Wetangula na Musalia Mudavadi akisema walichagua kumuunga mkono wakati mambo yalikuwa magumu sana.

Katika ibada hiyo naibu wake Rigathi Gachagua amesisitiza kuwa wahubiri lazima wataendelea kumiminika katika ikulu ra rais licha ya wanaolalamikia dini kuwa na nafasi kubwa katika ikulu.

Rigathi amesema kuwa hata kama maafisa wa usalama watawazuia wahubiri na wainjilisiti kuingia Ikulu itambidi mkewe rais Mama Rachael Ruto kuwafungulia malango.

Naibu rais amewataka wakenya kumuombea rais kwa Mungu apate uwezo wa kuongoza taifa la Kenya linalokumbwa na matatizo makubwa kwa sasa. Gachagua ambaye pia anahitaji maombi ili kuweza kutekeleza majukumu yake amesema watu wengi wanakumbwa na matatizo mbali mbali na vyema kuomba kama taifa ili kukumbana na changamoto hizo.

Subscribe to eNewsletter