Local Bulletins

Wizara ya Afya yatazamiwa kuzindua kampeni ya siku 100 ili kuongeza utoaji wa chanjo kote nchini.

Picha:Hisani

Na Grace Gumato,

Wizara ya Afya inatazamiwa kuzindua kampeni ya siku 100 ili kuongeza utoaji wa chanjo kote nchini.

Msukumo wa Mpango wa Kitaifa wa Chanjo wa Wizara ya afya (NVIP) kwa msaada kutoka kwa washirika unalenga watoto wanaostahiki, wanawake wa umri wa kuzaa na wajawazito ambao walikosa huduma muhimu za kawaida za chanjo wakati wa janga la Covid-19.

Wasichana wenye umri wa kati ya miaka 10-14 na watu wazima wanaostahili wanatakiwa kutembelea kituo cha afya kilicho karibu nao ili kupokea chanjo zinazokusudiwa.

Maafisa wa Wizara na washikadau watafanya mkutano wa uhamasishaji hii leo ili kuangazia mikakati ya kufikia wazazi, viongozi wa jamii na viongozi wa kisiasa ili kuharakisha utoaji wa chanjo ili kupunguza viwango vya maradhi na vifo vya magonjwa yanayozuilika kwa chanjo.

Kampeni hiyo inakuja kufuatia wasiwasi wa viwango vya chini vya chanjo tangu mwaka jana.

Nchini Kenya, Covid-19 ilitatiza kwa kiasi kikubwa huduma za kawaida za chanjo na shughuli za uchunguzi, na kutishia mafanikio katika kutokomeza polio na kutokomeza magonjwa yanayoweza kuzuilika.

Kulingana na Shirika la Afya Ulimwenguni, kumekuwa na punguzo kidogo, la karibu asilimia 5 ya chanjo mwaka 2020.

Hii ilitokana hasa na changamoto zinazoletwa na janga la COVID-19, ikiwa ni pamoja na upatikanaji wa vituo vya afya kutokana na vikwazo vya kutembea na hofu ya kuambukizwa virusi.

Subscribe to eNewsletter