Local Bulletins

Jaji Mkuu David Maraga astaafu rasmi na kuwataka majaji kutekeleza wajibu wao kwa uadilifu

Aliyekuwa Jaji Mkuu David Maraga akiaga idara ya mahakama nje ya majengo ya mahakama ya Juu

Jaji mkuu David Maraga amestaafu rasmi kama jaji mkuu baada ya kuhudumu kwa miaka minne kama jaji mkuu.

Maraga ambaye amehudumu kama jaji wa mahakama kuu kwa zaidi ya miaka 18 atakumbukwa kwa mengi hususani uamuzi wake wakufutilia mbali uchaguzi wa urais wa mwaka wa 2017.

Katika hafla ilioandaliwa katika mahakama ya upeo jijini Nairobi jaji mkuu mstaafu Maraga amemkabidhi rasmi naibu wake Philomena Mwilu wadhfa huo kabla ya idara ya mahakama kumteua jaji mkuu mpya kwa kipindi cha miaka minne ijayo.

Katika hotuba yake ya mwisho Maraga ametoa wito kwa maafisa wa idara ya  mahakama kutekeleza majukumu yao kwa ujasiri bila uoga na mapendeleo.

Amewataka kuzingatia sheria na katiba ya taifa na kumuomba Mungu kwa kila jambo.

Jaji huyo mstaafu alikiri kwamba safari yake kama Jaji mkuu haikuwa rahisi na kwamba alipokea vitisho chungu nzima kutokana na kazi yake.

Kaimu jaji mkuu Philomena Mwilu amesifia utendakzi wa Maraga na kuahidi kuendeleza kazi zilizoasisiwa na mtangulizi wake.

Jukumu la mwisho la Maraga limekuwa jana asubuhi alipoongoza kikao cha mahakama ya juu kilichoandaliwa kwa heshima yake.

Hafla ya kustaafu kwake ilihudhuriwa na familia yake, viongozi wa makanisa, mawakili na majaji.

Katika hafla hiyo ya kufana nje ya makao makuu ya mahakama ya juu Maraga alivuliwa nguo zake rasmi za kazi na gari lake likaondolewa nambari rasmi za Jaji mkuu ‘CJ 1’ na bidhaa  hizo zote zilikakabidhiwa msajili mkuu wa mahakama Anne Amadi.

Maraga alichukua hatamu za kuongoza idara ya mahakama mwaka 2016 baada ya kustaafu kwa jaji mkuu Willy Mutunga.   Amekua jaji mkuu wa 15 katika historia ya Kenya.

Subscribe to eNewsletter