Local Bulletins

Nyani watengenezwa kitoweo kufuatia makali ya njaa, Lomelo kaunti ya Turkana

Nyani aliyewindwa na sasa anaandaliwa kitoweo.

BY MACHUKI DENNSON

Wenyeji wa eneo la Lomelo kaunti ndogo ya Turkana mashariki wameamua kuwinda na kula nyani baada ya kuzidiwa na njaa kwa muda sasa.

Wakaazi hao wanasema wamekosa namna na hivyo kuwabidi kuanza kula wanyamamwitu kama nyani.

 Wanasema kwamba kwa sasa hawana mifugo kwao baada ya kuvamiwa na jamii jirani iliyowapokonya kila kitu ijapokuwa wanambuzi pekee.

 Kulingana na mwalimu Julius Naukot wenyeji hao ambao wanaishi karibu na mto Suguta ambao una maji ya chumvi wamesalia hohe hahe kutokana na ukosefu wa usalama katika eneo hilo.

Nyani aliyeteketezwa kwa ajili ya kuandaliwa kitoweo kule Lomelo, Turkana.

Mwalimu ameiambia Jangwani kwamba wanawinda nyani na kisha kumchoma kabla ya kubeba kuenda nyumbani kuchemsha au kuchoma na kula sawa na nyama choma nyingine ile.

Chifu wa Lomelo Jackson Ekwang amethitisha hali hiyo akisema kwamba ujumbe wa hali mbaya ya njaa katika eneo hilo la Lomelo umewafikia maafisa wakuu wa serikali na bado wanasubiri kuona hatua itakayochukuliwa.

 Chifu Ekwang anasema kwamba katika eneo hilo hakuna hata shirika lisilo la kiserikali NGO, kutokana na hali mbaya ya usalama.

NGO ya mwisho iliyokuwa katika eneo hilo ilikuwa mwaka wa 2017 iitwayo ACTED na chifu anasema kwamba maafisa wa shirika hilo walivamiwa mara nyingi na wakalazimika kuhama kwa kuhofia kuawa.

Mwalimu Naukot ameiambai Radio Jangwani mara ya mwisho watu katika eneo hilo kupokea chakula cha msaada ilikuwa mwezi Februari mwaka huu kutoka kwa serikali ya kaunti ya Turkana.

Aidha mwaka jana pia walipokea chakula cha msaada kutoka kwa shirika la msalaba mwekundu.

Mzoga wa nyani.

Mwalimu anasema kwamba chakula walichopokea mwezi wa pili hata hivyo kilikuwa kidogo sana kuwamudu kwa muda.

 Anasema kwamba walipewa gunia moja la kilo 50 kwa familia tatu bila ya kujali familia moja ina watu wangapi.

 Tangu mwezi wa pili hadi kufikia sasa hawajaona msaada wowote na wanahofia kuondoka sehemu kuenda kutafuta chakula kutokana na kwamba watavamiwa.

Kamisha wa kaunti ya Turkana Wambua Muthama amekanusha taarifa za watu kuangamia kutokana na njaa katika eneo la Lomelo akisema kwamba mvua imenyesha maajuzi na kwa sasa wanafaa kuwa na chakula.

Aidha amesema afisi yake haijafahamishwa kuhusu janga hilo.

Eneo hilo nla Lomelo karibu na  mto Suguta ndiko mahali maafisa wa polisi watu waliuawa na wengine 14 kujeruhiwa hivi maajuzi.

Lomelo iko katika mpaka wa kaunti ya Turkana na Baringo jamii jirani ikiwa ile ya Pokot.

Subscribe to eNewsletter